Jumla ya Shilingi Bilioni 19,171, 601, 509. 00 zinatarajiwa kutumika katika ujenzi wa Kituo Kikuu cha Mabasi cha Geita Mjini, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Mradi wa Uboreshaji wa Miundombinu ya Miji Tanzania kwa awamu ya Pili (TACTIC 2) ambapo kukamilika kwake kunatarajiwa kuongeza mapato ya Halmashauri hiyo kutoka shilingi Milioni 172, 612, 045.29 hadi kufikia 274,124, 207.43 kwa mwaka.
Wakati wa utiaji saini wa Mkataba huo leo Juni 06, 2025, mhandisi Humphrey Kanyenye, Mratibu wa mradi wa TACTICS ameeleza kuwa Mradi wa Ujenzi wa Kituo hicho cha mabasi unatekelezwa kwa kipindi cha miezi 15 na Mkandarasi M/s Sihotech Engineeering Company Ltd kwa kushirikiana na AMJ global Mult Contractors, ukihusisha pia ujenzi wa wa barabara za kuingia na kutoka katika eneo la Magogo, panapojengwa kituo cha mabasi.
“ Ujenzi wa Kituo hiki cha kisasa cha mabasi utakuwa ni wa jengo la ghorofa mbili, barabara za kuzunguka kituo hicho cha mabasi zenye jumla ya Kilomita 1.6 za kiwango cha lami, kumbi za abiria kuketi, ofisi za usimamizi na uendeshaji, maduka, chumba cha faragha cha mama na mtoto, vyumba vya sala pamoja na kisima cha kutunzia maji ya mvua na maegesho ya magari, bajaji na pikipiki, “alisema Kanyeye
Awali katika maelezo yake kuhusu utekelezaji wa mradi wa TACTIC awamu ya kwanza katika Manispaa hiyo, Kanyenye amebainisha kuwa utekelezaji wake hauridhishi, ukiwa umefikia asilimia 45 ilihali mwisho wa utekelezaji wake ukitakiwa kufikia mwisho Mei 19, 2025, akieleza kuwa kwasasa wamelifikisha suala hilo kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali ili kuweza kusitisha Mkataba na Mkandarasi M/s Sichuan Road ans Bridge Group Corporation Ltd ambaye anatekeleza ujenzi wa barabara za mjini kati zenye urefu wa Kilomita 17 na jengo la usimamizi na uratibu wa mradi huo.
Akizungumza katika hafla ya utiaji saini mradi huo, Mstahiki Meya wa Manispaa ya Geita Mhe. Constantine Moland amebainisha kuwa kutekelezwa kwa mradi huo kunarejesha imani ya wananchi kwa Madiwani wa Manispaa hiyo, akieleza kuwa awali walikuwa wakionekana kama Madiwani hakuna ambacho wamewahi kuahidi kikatekelezeka, hivyo amewataka Madiwani wa Halmashauri hiyo kutembea kifua mbele kwani mradi huo sasa rasmi umeanza kutekelezwa.