Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI Mhe. Mohamed Mchengerwa amesema kuwa, uchaguzi wa wanafunzi wa kujiunga na Kidato cha Tano na Vyuo umefanyika kwa kuzingatia ufaulu na nafasi zilizopo, hivyo hakutakuwa na fursa ya kufanya mabadiliko yoyote ya shule kutokana na ukosefu wa nafasi za kufanya mabadiliko hayo.
Waziri Mchengerwa amesema hayo leo Jijini Dodoma wakati akitoa taarifa kwa umma kuhusu uchaguzi wa wanafunzi wa kujiunga na kidato cha tano na vyuo vya elimu ya ufundi kwa mwaka 2025.
Waziri Mchengerwa amesema jumla ya wanafunzi 214,141 wakiwemo wasichana 97,517 na wavulana 116,624 wamechaguliwa kujiunga na Kidato cha Tano na Vyuo vya Elimu ya Ufundi ikijumuisha wanafunzi 1,028 wenye mahitaji maalum
“Muhula wa kwanza kwa wanafunzi wa Kidato cha Tano utaanza tarehe 08 Julai, 2025, waliopangwa wanapaswa kuanza kuripoti shuleni kuanzia tarehe 06 Julai, 2025 na siku ya mwisho ya kuripoti ni tarehe 21 Julai, 2025, na waliopangwa kwenye Vyuo vya Elimu ya Ufundi watapokea maelekezo ya namna ya kujiunga kutoka katika vyuo walivyopangiwa,” Mhe. MChengerwa amesisitiza.
Akizungumzia ubora wa ufaulu kwa kuangalia madaraja, Mhe. Mchengerwa ameainisha kuwa, watahiniwa 223,372 (41.23%) walipata ufaulu wa Daraja la I – III, hali inayoonesha kuwa ufaulu wa watahiniwa wa mwaka 2024 umeongezeka kwa asilimia 5.36% ikilinganishwa na ufaulu wa Daraja la I – III wa watahiniwa 198,394 (35.87%) wa mwaka 2023.
Aidha, Waziri Mchengerwa amewapongeza wanafunzi wote waliochaguliwa kujiunga na Kidato cha Tano na Vyuo vya Elimu ya Ufundi na kuwahimiza kuendelea kufanya bidii katika kujifunza ili waweze kufanikiwa kujiunga na mafunzo ya Elimu ya Juu baada ya kuhitimu Kidato cha Sita na Vyuo vya Elimu ya Ufundi.
Sanjari na hilo, Mhe. Mchengerwa amewapongeza walimu, wazazi na walezi wote kwa juhudi walizozifanya katika malezi na ufundishaji hali iliyowezesha wanafunzi kufaulu vizuri, na amewataka kuendelea kuwa na moyo wa kusimamia na kufuatilia maendeleo ya watoto shuleni.
Uchaguzi wa Wanafunzi wa Kujiunga na Kidato cha Tano katika Shule za Sekondari na Vyuo vya Elimu ya Ufundi vya Serikali umefanyika kwa kuzingatia utekelezaji wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 toleo la 2023 na Mtaala ulioboreshwa, hivyo wanafunzi waliochaguliwa ni kutoka Shule za Serikali, zisizo za Serikali na watahiniwa wa kujitegemea waliofanya mtihani chini ya Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima.