WADAU MADALE GROUP WAZINDUA SACCOS YAO


Kikundi cha Wadau Madale kimefanya hafla ya uzinduzi wa Saccos yao ili kuondokana na utaratibu wa kuchangishana wakati wa matatizo sanjari na kujiinua kiuchumi.

Hafla ya uzinduzi wa Saccos hiyo imefanyika Jana Jumamosi Desemba 9, 2023 Lemoon Madale Jijini Dar es Salaam.

Akizungumza kwenye Mkutano Mkuu wa mwaka ulioambatana na uzinduzi wa Wadau Saccos Mwenyekiti wa wadau Group Stephen Kazimoto, amewataka wanachama wa Wadau Group kushiriki kikamilifu kwenye shughuli mbalimbali zinazoandaliwa na viongozi hatua itakayosaidia kukuza maendeleo ya umoja wao. 

Kazimoto amesema kuwa kwa mwaka utakaoanza 2024 hawatapenda usumbufu kila Mwanachama anapaswa ajitambue ili tuzidi kusonga mbele.

“Tangu kuanzisha kwa umoja huu wa wadau mwaka 2014 hadi Sasa kikundi kimesimama kwasababu ya sisi viongozi kutenda haki kwa kila mmoja anapopata shida”, amesema Kazimoto

Ameeleza kuwa walijenga kituo cha Polisi ambacho kinasimamiwa na Mzee Mponja ambapo walitumia fedha za wanakikundi shilingi Milioni 250, Kituo hicho ujenzi haujakamilika hivyo amewaomba wanakikundi wenzie kufanya jitihada ili waweze kikimalizia.

Kwaupande wake Afisa Ushirika Manispaa ya Kinondoni Jijini Dar es Salaam Zahara Kamtande, amesema Saccos ni miongoni mwa vyama vya ushirika ambavyo vinajiunga kwa hiari ili kujikwamua kiuchumi. 

Amesema Ushirika unaendeshwa na sheria namba 6 ya vyama vya ushirika ya mwaka 2013,namba ya uendeshaji wa vyama vya ushirika umefanana karibia nchi nzima ila ushirika wa akiba na mikopo upo tofauti na vyama vingine.

“Kwenye ushirika wa akiba na mikopo kunasheria iliyoongezwa ambayo ni sheria ya huduma ndogo za fedha namba 10 ya mwaka 2018 hii sheria inaelezea namna ambavyo vyama vya ushirika wa akiba na mikopo inavyoshindana na taasisi zingine za fedha ambayo inasimamiwa na kanuni ya huduma ndogo ya fedha ya mwaka 2019”,

Ameeleza kuwa ili Sacoss yoyote iweze kujiendesha ni lazima kuwepo na kiingilio ambacho kitasaidia kujenga mtaji wa chama na Mwanachama akilipia kiingilio na akataka kujiondoa fedha hiyo hairudishwi.

Post a Comment

Previous Post Next Post