DKT.ABBASI AIPONGEZA TFS KWA MAPINDUZI YA MAPATO ASEMA SEKTA YA MISITU NI MUHIMILI WA TAIFA


Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Dkt. Hassan Abbasi, ameipongeza Taasisi ya Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kwa kuonesha mageuzi makubwa ya kiutendaji, kuongeza mapato na kuifanya sekta ya misitu kuwa mhimili muhimu wa uchumi wa taifa.

Akifunga rasmi Mkutano wa Nne wa Viongozi na Makamanda wa Vituo vya TFS Februari 23, 2026 katika Ukumbi wa Hoteli ya Cate, Morogoro, Dkt. Abbasi amesema mafanikio ya taasisi hiyo yanaonesha kuwa misitu si sekta ya pembezoni bali ni injini ya maendeleo ya uchumi, afya, maji na mazingira.

Kwa mujibu wa takwimu zilizotolewa katika mkutano huo, mwaka wa fedha uliopita TFS ilikusanya zaidi ya Sh. bilioni 189 dhidi ya lengo la Sh. bilioni 176, na hadi kufikia Februari mwaka huu, tayari ilikuwa imekusanya Sh. bilioni 127 sawa na asilimia 70 ya makadirio ya mwaka ikiwa ni mapato kutoka vyanzo vya ndani.

Katika soko la nje, mauzo ya mazao ya misitu yamefikia Sh bilioni 196.9, huku asali tani 1,596 zikiuzwa nje kwa thamani ya Sh bilioni 19.2.

Dkt. Abbasi alisema ongezeko hilo ni ishara ya mabadiliko ya kimkakati ndani ya taasisi.

Aidha, aliipongeza TFS kwa kuwekeza katika utalii ikolojia ndani ya hifadhi za misitu, akisema idadi ya watalii imeongezeka kwa kasi kutoka watalii 59,606 mwaka 2020/2021 hadi 346,394 kwa sasa. Huku mapato yakiongezeka kutoka Sh 154,965,050 hadi Sh 2,884,549,246, hatua inayoonesha ukuaji mkubwa wa sekta hiyo ndani ya taasisi.

“Hii inaonyesha misitu si kwa ajili ya miti tu, bali ni rasilimali ya kiuchumi,” alisisitiza.

Dkt. Abbasi alisema sekta ya misitu sasa inachangia asilimia 3.4 ya Pato la Taifa, ikiendelea kuwa nguzo muhimu katika mapambano dhidi ya mabadiliko ya tabianchi na ulinzi wa vyanzo vya maji.

Post a Comment

Previous Post Next Post