Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Mhe. Daniel Chongolo, ameongoza kikao cha Baraza la Madiwani cha kujadili hoja zilizobainishwa katika ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi leo tarehe 10 Juni 2025.
Kikao hicho kimehudhuriwa na Mkuu wa Wilaya ya Mbozi, Kamati za Ulinzi na Usalama za Mkoa na Halmashauri, wataalamu wa halmashauri pamoja na Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi.
Katika kikao hicho, Mhe. Chongolo amewapongeza madiwani wa Halmashauri ya Mbozi kwa kazi kubwa wanayoifanya katika kusukuma maendeleo ya wananchi. Akiwaeleza washiriki wa kikao, Mhe. Chongolo alisema:
“Mambo mengi tuliyoyajadili mwaka jana yamepungua, hoja nyingi zimepungua. Hii ndiyo kazi ambayo wataalamu tunatakiwa kuifanya. Mimi niwapongeze sana.”
Aidha, aliongeza kwa kueleza kuwa Mkoa wa Songwe umeendelea kuwa miongoni mwa mikoa iliyopata fursa ya kupokea bajeti ya maendeleo kwa asilimia mia moja kwa kipindi cha miaka minne mfululizo, na tena kwa wakati.
“Mkoa wetu umepata bahati kwa kipindi hiki chote cha miaka minne umekuwa ukiletewa bajeti ya maendeleo kwa asilimia mia moja, na kwa mapema sana. Hii bajeti ya maendeleo ndiyo inayo tafsiri dhamira ya Serikali chini ya Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuboresha huduma kwa wananchi wetu,” alisisitiza Mhe. Chongolo.
Kikao hicho ni sehemu na juhudi za serikali kuhakikisha uwajibikaji, ufanisi na utekelezaji wa majukumu ya halmashauri unafanyika kwa weledi na kwa manufaa ya wananchi.