DKT.KIRUSWA AKAGUA MGODI WA TANZANIA - ZAMBIA DINGTAI


Naibu Waziri wa Madini Dkt.Steven Kiruswa Juni 2, 2024  alikagua mgodi wa Tanzania- Zambia DingTai Mining Co. Ltd ulioingia makubaliano ya kutoa msaada wa kiufundi kwenye leseni za uchimbaji mdogo 36 zinazomilikiwa na Waziri Gao, Aisha Waziri Gao na Chama cha Ushirika Mgusu zilizopo katika eneo la Saragulwa mkoani Geita.

Mbali ya  kukagua, Waziri alifanya kikao  kilichojumuisha menejimenti ya mgodi huo unaotarajia kuanza uchimbaji wa madini ya dhahabu siku za karibuni.

Akizungumza katika kikao hicho , Dkt.Kiruswa aliupongeza mgodi  ulipofikia  na kuutaka mgodi  kuongeza matumizi ya teknolojia katika uchimbaji na uchenjuaji  madini ili kuweka mazingira salama katika eneo la mgodi.

Akielezea kuhusu utaratibu wa  ushirikishwaji wa jamii inayozunguka mgodi , Dkt .Kiruswa aliutaka mgodi kutekeleza mpango wa Ushirikishwaji wa Jamii inayozunguka mgodi ikiwa ni takwa la kisheria la kushirikisha jamii katika masuala yote ya kimkakati yanayohusu shughuli za maendeleo katika eneo la mgodi.

Akifafanua juu ya utunzaji wa mazingira katika eneo la mgodi Dkt. Kiruswa aliutaka mgodi kuzingatia utunzaji mazingira ndani na nje ya mgodi kama kanuni , taratibu na sheria zinavyoelekeza.

Naye, mmiliki wa baadhi ya leseni zilizoingia ubia huo  Ahmed Waziri Gao alisema mgodi unatarajia kuzalisha kiasi cha kilogramu 50 za dhahabu kwa mwezi na kuchangia mrabaha  wa Shilingi Milioni 280 kwa mwezi.

Gao aliongeza kuwa lengo la mgodi ni kuhama kutoka uchimbaji mdogo kwenda uchimbaji mkubwa pindi taratibu na mipango ya uzalishaji itakapo kamilika.

Akielezea kuhusu ajira ndani ya mgodi , Gao alisema kuwa mpaka sasa mgodi umeajiri wafanyakazi wazawa 48 wanaofanyakazi katika vitengo mbalimbali ndani ya mgodi.

Post a Comment

Previous Post Next Post