Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya Dkt. John Jingu amewawaagiza watumishi na wataalam wote wa Afya nchini kuimarisha mahudhurio kwa kuhakikisha wanakuwepo maeneo yao ya kazi kwa muda stahiki wanaotakiwa kuwapo ili kukabilina na majukumu yao na kuiepusha jamii na madhila ambayo yanaepukika.
Dkt.Jingu ameyasema hayo Juni 9, 2024 wakati wa ziara yake ya kushtukiza aliyolenga kujionea hali ya utoaji wa huduma na shughuli zinavyoendelea katika Taasisi ya Tiba ya Mifupa na Ubongo Muhimbili (MOI) Jijini Dar es Salaam, na kusisitiza kuwa katika sekta ya afya uzembe mdogo unaleta madhara makubwa kwa jamii na taifa kiujumla.
"Mtu kutokuwepo kazini kwa mujibu wa Sheria na taratibu za utumishi wa umma ni kosa, na hauikubaliki, Watu wanatakiwa wawepo kazini katika maeneo yao ya kazi mda wote wanaopaswa kuwepo, na watu wajisajiri kwenye biometric wanapoingia na kutoka, lakini pia tuzingatia miongozo inayotuongoza katika kutoa huduma tumeona pale kuna shida katika eneo hilo." Amesema Dkt. Jingu
Dkt Jingu ameongeza kuwa wataalamu hao wawapo katika majukumu yao pia ni muhimu kuzingatia na kufuata miongozo inayowaongoza katika kutoa huduma za matibabu.
"Afya ni tofauti na vitu vingine kosa, kwani likifanyika wakati mwingine halina dawa, uzembe mmoja ama kutowajika kidogo kunaweza pelekea mtu akapoteza maisha au mtu akapata ulemavu ambao ungeepukika, sasa matokeo yake mtu anaendelea kupata maumivu ambayo yange epukika, Hivyo ni vyema kuzingatia ufanyaji kazi wa uweledi ili kuisaidia jamii yetu na taifa kwa ujumla" amesema Dkt. Jingu
Nae Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Tumaini Nagu ametumia fursa hiyo kusisitiza watoa huduma za afya nchini kuhakikisha wanaweka kipaumbele huduma kwa mgonjwa na sio Fedha.